
Hivi karibuni kumeibuka mtindo wa wasanii wa kike na hata wa kiume
kupata shutuma za aina mbali mbali ambazo nyingi kati ya hizo ziko
kwenye mrengo wa maisha ya mtu ya ndani ambayo mara nyingi yanatakiwa
kubaki kwa mtu mwenyewe.
Hapa tunamaanisha masuala yote yanayohusu faragha ya ndani kama
masuala ya ndani ya kimahusiano, maadili, staha, utu na heshima ya mwili
wa mtu au watu. Kwa bahati mbaya tangu masuala haya yameanza kuibuka
hayapungui, bali yanazidi kuongezeka.
Kwa asilimia kubwa upande wa faragha ya matendo yanayohusiana na
mahusiano na faragha ya viungo vya wahusika ndio vimekuwa ajenda kubwa
katika vyombo vya habari. Matukio hayo yamekuwa si haba kujadiliwa
katika mitandao ya kijamii pamoja na kurasa za magazeti mbali mbali
karibu kila mwezi.
Tumeanza na maelezo hayo ili kujaribu kujadili yale yatokanayo na
aina hii ya fedheha au kadhia ambayo imeonekana kwamba Watanzania
wameanza kuichukia. Tutaanza na tukio la Diamond ambaye yeye alifanya
kile kisichotarajiwa kwa kuonyesha nguo zake za ndani katika jukwaa la
shoo ya Fiesta Dar-Es-Salaam kama ishara ya kuonyesha usafi wake.
Hapa cha kujiuliza je katika matendo yote ambayo Diamond angeweza
kuyafanya ili kuiaminisha jamii juu ya usafi wake, hili la kuonyesha
nguo za ndani ndio lilikuwa lenye umuhimu mkubwa kiasi cha kuamua
kufanya hivyo? Je hakukuwa na aina nyingine ya kubainisha hilo?

Jambo lingine ambalo linakera zaidi ni namna wasanii wa kiume ambavyo
wanapenda kuning’iza suruali ama kaptura zao (mlegezo). Wasanii hao
wengi wao ni wale wa muziki wa kizazi kipya wamekuwa na tabia ambayo
imekuwa inalalamikiwa sana ya kuvaa Jeans aina ya suruali na Kaptura
chini ya makalio.
Narudi kwa dada zangu ambao wao ndio wanaonekana wahanga wakubwa wa
matukio ya namna hii. Hatumaanishi kwamba tunataka kuwananga ama
kuwasimanga, la hasha bali tunalotaka kushauri ni namna wasanii iwe wa
muziki, filamu ama sanaa ambayo kwa namna moja ama nyingine inawafanya
kuwa karibu na jamii.
Ni aibu kubwa kwa msanii kufanya jambo ambalo kwa maudhui yake kama
hatakuwa na uwezo wa kulizuia lisidhuru heshima na haiba yake katika
siku za usoni akaliruhusu lifanyike. Hapa tunamaanisha kwa mfano
matumizi ya picha kwa kutumia aina yoyote ya camera iwe ya picha mgando
ama zenye motion.
Ukiangalia kwa ndani mambo mengi ya namna hii hutokana na mazoea
ambapo mtu huanza pole pole kwa kujipiga picha kisha akaziangalia
mwenyewe. Baada ya hapo atapiga picha na kisha kuziangalia na wenzake
mara nyingi huwa ni wale walioshibana wa jinsia moja.
Kisha tabia hiyo huanza kuenea kwenda kwa wapenzi wo. Hapa ndipo tatizo kubwa hutokea.
Shughuli ya faragha huanza kupungua kadiri siku zinavyokwenda ambapo
mtu na rafiki zake huanza kuonyeshana picha hizo ambapo mpenzi wa kiume
naye huanza kuwaonyesha maswahiba zake wa karibu na kisha kwa kutegemea
uimara ama hatua ya uhusiano uliopo kati ya wahusika hao wote basi
athari hujitokeza pale uhusiano huo baina ya watu hao utakapoharibika.
Upande mmoja wapo katika hali ya kukomoa ama kulipa kisasi huamua
kuzisambaza kwa jamii kwa sababu anajua madhara ambayo yatamkuta
mlengwa. Ushahidi wa hili lipo kwenye picha za mwanadada ambaye
alishiriki video ya Masogange, Agnes.

Hatutaki kuingia kwa undani kuhusiana na suala hilo ila matokeo yake wote mnayajua.
Mwingine ambaye yamemkuta maswahibu ya namna hii ni pamoja na msanii
wa muvi za kibongo Rayuu ambaye yeye kwa utashi wake ambao ni ngumu
kuuelewa aliweka picha zake zikionyesha tattoo zilizoenea katika maeneo
mbalimbali katika sehemu kubwa zaidi ya mwili wake, kitendo
kilichoamsha majibizano makali kati yake na mdau mwingine wa tasnia ya
filamu Sintah ambaye alihisi wao kama kina dada wamedhalilishwa na
msichana mwenzao.

Pili uvaaji wa dada zetu ndio kichocheo kikubwa cha matatizo
haya.Haiwezekani kwa akili ya kawaida tu mtu kuvaa nguo fupi isiyositiri
faragha kwa asilimia 90 katika tafrija, sherehe ama shoo ya kijamii na
kutegemea kwamba hali itakuwa shwari. Wema na Aunt Ezekiel ni mashuhuda
wazuri katika hili.
Hatuna uhakika kama Aunt wakati analitolea utetezi suala hili
alilifikiria kwa umakini wa hali ya juu na kusema waandishi wa habari
wamekuwa wanawavizia chini ya jukwaa ili wawapige picha zitakazo
onyshesha nguo za ndani.
Tunatambua kazi ya kueleimisha ama kuikosoa jamii ni ngumu lakini
tunapenda kusema kwa hili itabidi dada zetu wabadilike kwani hawana ma
jeans au nguo ndefu itakayofunika ugoko na kuondoa kadhia hiyo. Je ni
lazima msanii avae nguo fupi sana kila wakati anapokuwa katika tafrija
ya aina yeyote ile, ikiwemo na kwenye ku act?
Tunafikiri kama sio picha zile zilizowaonyesha Wema na Aunt Ezekiel
namna ile, basi Jukwaa la fiesta jijini Dar-Es-Salaam lingekuwa na
viroja kwani siku ile wengi wa wasanii walikuwa na tahadhari ya hali ya
juu na kuamua kuvaa tofauti na hisia zao huwa zinavyowatuma.
Tulimwona jinsi Shilole alivyokuwa mwangalifu na hata ilimbidi kuvaa
nguo ambayo ilimkwepesha na dhahama za picha chafu. Yeye pamoja na
madensa wake walibadili aina ya nguo ambazo mara nyingi hutumia kwenye
shoo zake.

Shilole akiwa jukwaani kwenye Fiesta Dar
Wasanii wanatakiwa watambue maana ya kudumisha uhusiano mzuri na
jamii, usio na mikwaruzano ya ki itikadi, hisia, jinsia, dini, kabila
wala fikra. Ingekuwa katika nchi nyingine tUnafikiri wasanii kama
Diamond, Aunt Ezekiel na Wema sepetu wangepoteza nafasi zao za kibalozi
kama wangekuwa nayo kama alivyo Diamond na ubalozi wa utalii.
Tunakumbushia tu…..Faragha ni kitu muhimu katika kulinda utu, kudumisha heshima na kustawisha maadili katika jamii.
Source: Vituko vya Mtaa