INSIDE INAPATIKANA MADUKANI

FILAMU YA JADA ITAKUWA SOKONI 19.02.2015

JADA IPO SOKONI

JADA IPO SOKONI

Wednesday, March 4, 2015

KAPTENI JOHN KOMBA KIMYA MILELE



Waandishi wetu/mchanganyiko11
NIKIMYA Milele. Hivyo ndivyo unavyoweza kusema baada ya msiba mkubwa uliotingisha nchi, kufuatia kufariki ghafla, kuagwa na hatimaye kufanyika kwa mazishi ya Mbunge wa Mbinga Magharibi, Kapteini Mstaafu wa Jeshi, John Damian Komba katika Kijiji cha Lituhi, kilichopo katika mwambao wa Ziwa Nyasa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Risasi Mchanganyiko lina habari kamili.


Mwili wa Kapteini John Damian Komba ukiagwa.

ALIVYOAGWA
Kapteni Komba aliyekuwa pia ni mtunzi mahiri wa nyimbo na mwimbaji hodari wa kwaya, kabla ya mazishi yake, aliagwa katika tukio la kitaifa lililofanyika kwenye Viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi wote wakubwa, wakiongozwa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Makamu wake, Dokta Ghalib Bilal na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anne Makinda.

WANAOTAJWA URAIS 2015 WAMUAGA
Wengine waliokuwepo katika tukio hilo lililorushwa moja kwa moja na kituo cha taifa cha televisheni cha TBC 1, ni wanaotajwa kuwania nafasi ya kuteuliwa kuwa Rais katika uchaguzi mkuu ujao kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja ambaye ni mbunge wa Sengerema.
Waombolezaji wakiuaga mwili wa marehemu kwa simanzi kubwa.

UKAWA NAO NDANI
Pia alikuwepo Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Dokta Wilbroad Slaa, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia wanaowakilisha Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na wabunge kutoka vyama vyote vya siasa, majaji wa Mahakama Kuu, marais wawili wastaafu, Ally Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa na viongozi waandamizi wa zamani na sasa katika serikali.

WANAOTAJWA URAIS AZUA GUMZO
Ingawa tukio hilo lilikuwa ni la huzuni, lakini bado wagombea hao wa Urais waliwateka mamia ya waombolezaji kutokana na wapambe wa pande zote mbili kujawa na hamasa walipokuwa wakipita au majina yao kutajwa na MC wa shughuli hiyo.
Kwa nyakati tofauti, wawania uongozi hao walionekana nyumbani kwa marehemu, Mbezi Beach na baadaye katika ukumbi wa Karimjee.

WASANII WAINGIA MITINI KUAGA
Wakati hali ikiwa hivyo kwa wanasiasa wa kambi zote kuelezea kuguswa kwao na msiba huo wa mmoja wa watunzi hodari zaidi nchini, upande wa wasanii, walionekana kukwepa kuhudhuria hafla hiyo, tofauti na inavyotokea pale mwenzao anapofariki dunia. Ukiondoa wasanii walioalikwa kuimba, wakiwemo wa dansi, Bongo Fleva na Bongo Movies, hakukuwa na idadi kubwa ya mastaa hao kama ilivyotegemewa.

WALIOGOPA KUFUNIKWA NA WANASIASA?
Ilielezwa chinichini kuwa wasanii hao ambao mara zote hushindana kwa vituko, vibweka na matukio, walihofia kufunikwa na wanasiasa, ambao bila kujali tofauti zao za kiitikadi, waliomboleza kwa uzito uliostahili.

“Hawa sijui Bongo Movies, sijui Bongo Fleva hapa leo hakuna cha staa wala nini, mastaa wenyewe wanasiasa wamejazana, unafikiri wangekuja hapa wangemdengulia nani, wao ndiyo wangelazimika kuwa wanyonge na hivyo wanavyopenda kujikweza, wameogopa,” alisema mmoja wa waombolezaji hao.

LULU ATAWALA MITANDAONI
Aidha, msanii wa filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’ ambaye aliwahi kuzua minong’ono ya kutoka na marehemu, alijikuta katika wakati mgumu baada ya watu mbalimbali katika mitandao ya kijamii kumpa pole kwa msiba huo, ingawa wengi walionekana kumtania.


Rais Kikwete akiwa na huzuni.

LULU AWATOLEA UVIVU
Ili kuonyesha hasira aliyonayo, msanii huyo naye aliwajibu kwa kuwatolea maneno makali, ambayo kimaadili hayawezi kuandikwa gazetini. Gazeti hili lilijaribu kumtafuta binti huyo ili afunguke zaidi, lakini hakuweza kupatikana.Mama yake, Lucresia Karugila alipoulizwa, alisema jambo hilo ni la Lulu mwenyewe hivyo ni vyema akatafutwa mwenyewe.

MIGUNO MITANO
Kana kwamba haitoshi, waombolezaji walijikuta katika miguno mitano iliyoambatana na msiba huo wa aina yake. Mgono wa kwanza ulimhusu mwimbaji chipukizi wa THT, Ruby, aliyeimba wimbo wa Niongoze, ambaye alivaa nguo, japo nyeusi na ndefu, lakini ilikuwa ikionyesha sehemu ya mwili wake kutokana na wepesi wake.

MGUNO WA PILI
Mguno wa pili pia ulihusiana na nguo zilizovaliwa na msanii wa muziki Shilole, ambaye ingawa zilikuwa nyeusi na nzito, lakini ziliubana mwili wake kiasi cha kulifanya umbo lake lote kuonekana, kitu kilichowafanya waombolezaji kujikuta kwenye maswali yasiyo na majibu.


Rais mstaafu Benjamin Mkapa akiuzunika.

WA TATU
Mguno wa tatu uliotawala msiba huo, ni vitendo vya kimahaba vilivyofanywa na wasanii wapenzi, Jux na Vanessa Mdee, ambao muda mwingi wa shughuli hiyo walionekana wakishikanashikana pasipo kujali mazingira ya tukio hilo lililogusa jamii nzima ya Kitanzania.

WA NNE SASA!
Mguno wa nne katika hafla hiyo, ulihusu idadi ya watoto wa marehemu, waliotajwa kuwa 11, ambao baadhi ya waombolezaji walisema walisema ni wengi, huku wengine wakidai wachache. Hata hivyo, walimsifu kwa kitendo chake cha kuwalea vizuri na kuwaacha pasipo mfarakano kama inavyotokea misiba mingine.

WA TANO
Mguno wa mwisho uliotawala msiba huo ni juu ya chanzo cha kifo chake, kwani ingawa inafahamika kuwa ni shinikizo la damu, lakini baadhi yao wanasema inatokana na msongo wa mawazo, hasa kuhusiana na deni lake alilokuwa akidaiwa na benki ya CRDB.



Kapteini John Damian Komba enzi za uhai wake. Komba alitarajiwa kuzikwa jana katika Kijiji cha Lituhi, kilichopo katika mwambao wa Ziwa Nyasa wilaya ya Mbinga.Mungu ailaze roho ya marehemu Komba mahala pema peponi, Amina-Mhariri.

Imeandikwa na Musa Mateja, Imelda Mtema, Hamida Hassan, Shani Ramadhan, Chande Abdallah na Mayasa Mariwata.

No comments:

Post a Comment